MREMBO MISS TANZANIA AONGOZA WAKAZI WA DAR KATIKA ZOEZI LA UCHANGIAJI DAMU

Mshindi wa tatu wa Miss Tanzania 2014,Doris Mollel akishiriki zoezi la uchangiaji damu katika ikiwa ni sehemu ya kusherehekea Siku ya wanawake Duniani,iliyofanyika Buguruni Chama jijini Dar es Salaam mwishoni mwa wiki. Kushoto Ofisa Muuguzi kutoka Benki ya Damu Salama,Selina Joseph. Zoezi hilo la uchangiaji damu liliandaliwa na Mrembo huyo. 
 Mtoto wa Mkuu wa Mkoa wa Dar es salaam,Mh. Said Meck Sadick,Bi Mariam Meck Sadick akiungana na wananzania wengine kwenye zoezi la kuchangia damu ikiwa ni sehemu ya kumuunga mkono Mrembo Doris Mollel.
Baadhi ya wakazi wa jiji la Dar es Salaam wakishiliki zoezi la uchangiaji damu katika kusherehekea Siku ya wanawake Duniani,iliyofanyika Buguruni Chama jijini Dar es Salaam mwishoni mwa wiki.
Mpiga Picha wa Kampuni ya New Habari (2006) Ltd, John Dande akipima uzito tayari kwa kushiriki zoezi la uchangiaji damu,ikiwa ni sehemu kuunga mkono sherehe za Siku ya wanawake Duniani.zoezi hilo lilifanyika Buguruni Chama jijini Dar es Salaam mwishoni mwa wiki.Picha na John Dande.

Katika kuadhimisha siku ya wanawake duniani,mrembo Doris Mollel ambaye ni Miss Tanzania namba tatu kwa mwaka 2014 ameongoza mamia ya watanzania katika zoezi la kizalendo la kuhamasisha kuchangia damu kwa watanzania kwa ajili ya wagonjwa mbalimbali,zoezi ambalo limefanyika jijini Dar es salaam mwishoni mwa wiki. 
Zoezi hilo ambalo lilikuwa linaongozwa na mpango wa taifa wa damu salama kwa udhamini wa kampuni ya METL lilikuwa na lengo la kupata damu kwa ajili ya kuokoa maisha ya Mama na Mtoto kwani matatizo ya damu katika hospitali za Tanzania yamekuwa yakiongezeka siku hadi siku,jambo lililompelekea mrembo huyo kuamua kujitoa kuhamasisha watanzania kujitokeza kwa wingi katika zoezi hilo. 
Zoezi hilo lilifanyika Machi 8 mwaka huu katika maeneo ya Buguruni Chama kwa muda wa siku nzima,ambapo jumla ya uniti 65 za damu zimepatikana kiwango ambacho kimetajwa kuwa kinatia matumaini kwa mrembo huyo kufanikiwa katika kuwahamasisha watanzania kujitokeza kwa wingi. 
Akizungumza na wanahabari kuhusu kitu kilichomsukuma kuendesha zoezi hilo,Doris alisema kuwa ameamua kufanya hivyo baada ya kugundua kuwa wakina mama wengi pamoja na watoto hufariki dunia wakati wa kujifungua kutokana na kukosa damu ya kuongezewa,jambo ambalo amesema ni lazima watanzania kuungana kwa pamoja kutafuta damu ya kutosha katika kila hospitali ili kuiondoa hali hiyo ambayo inaweka hatarini maisha ya mama na mtoto wa kitanzania. 
Amesema kuwa swala la kujitolea damu ni swala la kizalendo zaidi na moyo wa kujitoa kwa kuwa kila mtanzania anaweza kuwa na uhitaji wa damu muda wowote hivyo ni lazima watanzania wawe na utamaduni wa kuchangia damu mara kwa mara kwani itasaidia endepo kutatokea uhitaji wa damu katika mahospitali yetu. 

Aidha amewataka watanzania wengine ambao wanauwezo wa kuhamasisha watu wengine kuchangia damu wafanye hivyo kwani kuna uhitaji mkubwa sana wa damu katika mahospitali ya kitanzania na kufanya hivyo ni kuokoa maisha ya watanzania wengi wenye uhitaji wa damu hiyo. 

Doris Mollel alijizolea umaarufu mwaka 2014 baada ya kufanikiwa kushika nafasi ya tatu katika shindano la Miss Tanzania mwaka huo ambapo aliwashinda warembo wengine waliokuwa wanawania taji hilo.